Saturday, December 31, 2016

UONGOZI WA SERIKALI YA MTAA WA MARUZUKU BUGURUNI JIJINI DAR ES SALAAM WATOA SARE ZA SHULE KWA WATOTO 200

Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Maruzuku katika Kata ya Mnyamani Buguruni Manispaa ya Ilala, kupitia Chama cha Wananchi (CUF), Jabiri Sanze (kulia), akimkabidhi sare za shule mtoto, Hamad Ali Dar es Salaamleo, ambaye ataanza darasa la kwanza mwezi huu. Serikali ya mtaa huo imetoa sare za shule, daftari na penseli kwa  watoto 200 watakaoanza darasa la kwanza mwaka huu wa 2017. Katikati ni mama wa mtoto huyo, Farida Rashid.
Mtoto Issa Athumani akipokea msaada huo. Katikati mama yake Halima Issa.
Mtoto Asnat Mashaka akipokea msaada huo. Nyuma yake ni mama yake, Arat Hamisi
Ofisa Mtendaji wa Kata ya Mnyamani Jafari Mrisho (kushoto), akizungumza kwenye tukio hilo.
Katibu Kata wa Kata ya Mnyamani (CUF), Omari Simba (kulia), akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo.
Wazazi na walezi wakiwa na watoto wao wakisubiri kupokea msaada huo.
Vifaa hivyo vikiandaliwa kabla ya kukabidhiwa watoto.
wazazi na walezi wakiwa kwenye hafla hiyo.
wazazi na walezi wakiwa kwenye hafla hiyo.
Watoto na wazazi wao wakisubiri msaada huo.
Na Dotto Mwaibale

SERIKALI ya Mtaa wa Maruzuku katika Kata ya Mnyamani Buguruni Manispaa ya Ilala kupitia Chama cha Wananchi (CUF), imetoa sare za shule kwa watoto 200 wanakaoanza darasa la kwanza mwezi Januari ili kuleta msukumo wa masomo katika mtaa huo.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi msaada huo Dar es Salaam leo, Mwenyekiti wa mtaa huo, Jabiri Sanze alisema wanaziunga mkono jitihada za Rais Dk.John Magufuli za kuhakikisha kila mwanafunzi anapata elimu bure na katika mazingira bora.

"Tumeamua kutoa msaada huu mdogo kwa watoto 200 waliopo katika mtaa wetu ili kutoa hamasa kwa wazazi na walezi kwani kipindi hiki cha mwezi Januari kinachangamoto kubwa na mahitaji mengi ya shule kwa wanafunzi" alisema Sanze.

Sanze alitaja msaada huo kuwa ni mashati ya shule, madaftari na penseli za kuandikia ambapo aliwaomba wazazi wasaidie eneo la sketi, kaputura, viatu na mabegi.

Alisema watoto walionufaika na msaada huo ni wavulana 86 na wasichana 114 wote kutoka katika mtaa wa Maruzuku.

Ofisa Mtendaji wa Kata ya Mnyamani Jafari Mrisho aliupengeza uongozi wa mtaa huo kwa mpango huo wa kuwasaidia watoto hao wanaotarajia kuanza darasa la kwanza na akawaomba wadau wengine wa maendeleo kujitokeza kusaidia ili kuwafikia watoto wote wa mitaa mitatu ya kata hiyo ambayo ni Mji Mpya, Mbarouk na Mnyamani.

Mjumbe wa mtaa huo Haroub Mussa aliwataka wazazi wa watoto waliopata msaada huo kutunza sare hizo na kuwa serikali ya mtaa itaendelea kushirikiana na wananchi na kuhakikisha watoto wote wanaopaswa kuanza darasa la kwanza wanakwenda shuleni.

No comments: