Sunday, July 31, 2016

DC IKUNGI AMTAKA DED WAKE KUMPA TAARIFA YA KUTOANZA UJENZI WA NYUMBA ZA WALIMU ZINAZOGHARAMIWA NA BENKI YA DUNIA

Mkuu wa wilaya ya Ikungi, Miraji Mtaturu akiwapungia mkono wananchi waliohudhuria kwenye uzinduzi wa uchagiaji wa damu salama,mfuko wa afya ya jamii(CHF) pamoja na daftari la ufuatiliaji akina mama wajawazito uliofanyika kwenye viwanja vya shule ya msingi Minyughe,wilayani Ikungi.
Mkuu wa wilaya ya Ikungi,Mkoani Singida,Miraji Mtaturu(wa kwanza kushoto) akimkabidhi Mbunge wa jimbo la Singida Magharibi(CCM), Elibariki Kingu daftari la ufuatiliaji akina mama wajawazito,mara baada ya kuzindua mpango huo uliofanyika kwenye viwanja vya shule ya msingi Minyughe,wilayani hapa.
Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Minyughe waliohudhuria uzinduzi wa uchangiaji wa damu salama lililofanyika kiwilaya katika kata ya Minyughe,tarafa ya Ihanja,wilaya ya Ikungi.
Mmoja wa wataalamu wa kitengo cha kukusanya damu salama akiwa katika jingo la darasa moja la shule ya msingi Minyughe,tarafa ya Ihanja wakati wa uzinduzi wa uchangiaji wa damu salama,mfuko wa afya ya jamii(CHF) na daftari la ufuatliji wajawazito kuhudhuria kliniki akikusanya chupa za damu zilizotolewa na wanafunzi wa shule ya sekondari ya kata aya Minyughe. (Picha Na Jumbe Ismailly).

Na. Jumbe Ismailly, Ikungi 


MKUU wa Wilaya ya Ikungi,Mkoani Singida amemuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo kuwa ifikapo Agosti mwaka huu ampatie taarifa za sababu zilizochangia Mkandarasi aliyepewa kazi ya ujenzi wa nyumba sita za shule ya msingi Minyughe kutoanza kazi kwa wakati uliopangwa ya ujenzi wa nyumba sita za walimu wa shule ya msingi Minyughe licha ya kupokea malipo ya kazi hiyo.

Mkuu huyo wa wilaya, Miraji Mtaturu alitoa agizo hilo katika Kijiji cha Minyughe, muda mfupi baada ya uzinduzi wa uchangiaji wa damu salama, mfuko wa afya ya jamii (CHF) pamoja na daftari la ufuatiliaji akina mama wajawazito uliofanyika kwenye viwanja vya shule ya msingi Minyughe,wilayani Ikungi.

Kwa mujibu wa Mtaturu kuchelewa kuanza kwa shughuli ya ujenzi huo wa nyumba za walimu utasababisha pia ukamilishaji wa nyumba hizo kutokamilika pia kwa wakati na huduma kwa walimu kucheleweshwa.

Akitoa taarifa kwa Mkuu huyo wa wilaya juu ya Mkandarasi kutoanza kazi za ujenzi wa nyumba hizo licha ya kupokea fedha za malipo ya shughuli hiyo, Mbunge wa jimbo la Singida Magharibi, Elibariki Kingu alisema miradi inayofadhiliwa na Benki ya dunia yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 750 katika Halmashauri hiyo imekwamishwa na Mkandarasi licha ya kulipwa fedha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba hizo za walimu, jambo linalosababisha walimu wa shule hizo kuishi katika nyumba zisizo na ubora unaotakiwa.

Hata hivyo Mbunge huyo kijana aliweka bayana kwamba baada ya kuonekana kila Mkandarasi anayetenda anatoa bei ya juu, yeye alimshawishi Waziri wa Tamisemi ili aweze kuiruhusu Halmashauri ifanye taratibu za manunuzi yenyewe ili kufanikisha shughuli hiyo iweze kufanyika mapema badala ya kuendelea kutegemea utaratibu wa wizara ambao unatumia fedha nyingi huku kukiwa na mwanya wa fedha za serikali kuliwa na baadhi ya watendaji wasiokuwa waaminifu.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo,Athumani Salumu akitoa utetezi wa sababu za kutoanza kwa shughuli hizo za ujenzi ni pamoja na ukosefu wa mchanga wa kuanzisha ujenzi wa nyumba hizo.

No comments: