Tuesday, September 30, 2014

TANZANIA KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA GIZ

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Michael John akitoa tamko kuhusu Siku ya Soko la Afya iliyoandaliwa na Wizara hiyo kwa kushirikiana na Shirika la GIZ , itakayofanyika Oktoba 2 katika ukumbi wa Diammond Jubelee jijini Dar es salaam.
Naibu Meneja wa Miradi ya Afya wa GIZ Bw. Christian Ptleiderer akizungumza na waandishi wa habari kutoa wito kwa mashirika mengine yanayotoa huduma za afya nchini kuendelea kusaidia na kusambaza huduma zao katika maeneo yenye changamoto ya miundombinu na uhaba wa watumishi wa afya.Kulia ni Mtaalam na Mawasiliano wa shirika la GIZ nchini Bi. Vida Mwasalla. Picha na Aron Msigwa – MAELEZO.

Na. Aron Msigwa – MAELEZO.

Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imesema kuwa itaendelea kushirikiana na Shirika la Ujerumani la GIZ katika uanzishaji na uendelezaji wa programu mbalimbali za utoaji wa huduma za afya zinazolenga kupunguza vifo vya watoto walio chini ya umri wa miaka 5.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Michael John ameyasema hayo leo jijini Dar es salaam wakati akitoa tamko kuhusu Siku ya Soko la Afya  nchini iliyoandaliwa na Wizara hiyo kwa kushirikiana na Shirika la Ujerumani la GIZ  itakayofanyika Oktoba 2,  jijini Dar es salaam.

Amesema Tanzania na GIZ zimekuwa zikishirikiana katika uboreshaji wa miradi mbalimbali ya afya kwa kusogeza huduma za afya karibu na wananchi kuanzia ngazi ya taifa, mikoa na Halimashauri za wilaya.

Ameeleza kuwa mikoa ya Lindi, Mbeya, Mtwara na Tanga imeendelea kunufaika na miradi mbalimbali ya ushirikiano  chini ya shirika hilo inayolenga kuimarisha miundombinu ya kutolea huduma za afya katika maeneo hayo, uimarishaji wa mifuko ya Afya ya Jamii na ushiriki wa moja kwa moja kusaidia upatikanaji na uendelezaji wa wataalam wa kutoa huduma za afya maeneo ya vijijini.

Ameongeza kuwa GIZ imekuwa ikishirikiana na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii katika kuhakikisha kuwa jamii inamudu huduma bora za afya kupitia Mifuko ya Hifadhi ya Afya ya Jamii iliyopo katika maeneo yao.

Aidha, amebainisha kuwa maonyesho ya siku ya Soko la Afya yatakayowahusisha wadau mbalimbali na mashirika yanayotoa huduma za afya nchini yanalenga kuwakutanisha wadau hao ili waweze  kujadili changamoto za utoaji wa huduma za afya nchni, kujifunza mafanikio yaliyopatikana katika baadhi ya maeneo na kuweka mikakati ya kuyafikia maeneo mengi zaidi.

Kwa upande wake Mtaalam na Mawasiliano wa shirika la GIZ nchini Bi. Vida Mwasalla ameeleza kuwa maonesho ya mwaka huu yazilenga Wizara, Taasisi , Washirika wa Maendeleo, Makampuni, Mashirika binafsi  na Wakala zinazojihusisha na utoaji na uendelezaji wa sekta ya afya nchini.

Amesema katika maonesho hayo GIZ kwa kushirikiana na Wizara ya Afya itaonyesha mikakati mbalimbali ya kuwaokoa watoto wadogo wenye matatizo ya afya, namna walivyofanikiwa kuwapata watumishi wa afya katika maeneo ya Lindi na Mtwara, maeneo  ambayo hapo awali walikuwa hawakai katika vituo vyao.

Ameongeza kuwa mbali na Siku ya Soko la Afya kuhusisha huduma za utoaji wa elimu, vipimo, machapisho mbalimbali inalenga kuwaweka pamoja wadau hao ili waweze kubadilishana uzoefu na kuweka  mikakati ya kuchangia maendeleo ya sekta ya afya hapa nchini.

Naye Naibu Meneja wa Miradi ya Afya wa GIZ Bw. Christian Ptleiderer ametoa wito kwa mashirika mengine yanayotoa huduma za afya nchini kuendelea kusaidia na kusambaza huduma zao katika maeneo ambayo bado yanakumbwa na changamoto mbalimbali za miundombinu na uhaba wa watumishi wa afya.


Amesema wao kama GIZ kwa kuanzia wameanza na mikoa 4, na wanaendelea kujenga uwezo wa kuyafikia maeneo mengi zaidi kwa kushirikiana na Serikali ya Ujerumani na Tanzania.

No comments: